Wednesday 29 March 2017

INAUZUNISHA:WAGONGWA NA NDEGE WAKATI WAKIPIGA SELFIE UWANJA WA NDEGE


Wanawake wawili wamepoteza maisha yao baada ya kugongwa na ndege walipokuwa wakipiga picha za selfie kwenye barabara inayotumiwa na ndege kutua katika uwanja wa ndege mjini Chinipas, Mexico.
Nitzia Mendoza na Clarissa Morquecho wenye umri wa miaka 18 na 17 mtawalia walikuwa wakipiga picha juu ya lori iliyokuwa imeegeshwa pembeni mwa barabara ya ndege walipogongwa na bawa la ndege na kufa papo hapo
Share:

RC Makonda ahojiwa na Kamati ya Haki, Kinga na Madaraka ya Bunge

Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, Paul Makonda, Jumanne hii ameanza kuhojiwa na Kamati ya Bunge ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge kujibu tuhuma zinazomkabili za kuingilia Haki, Uhuru na Madaraka ya Bunge.
Kwa mujibu wa maelezo kwenye akaunti maalum ya Facebook ya bunge hilo, wito wa kufika mbele ya kamati hiyo umefikiwa kufuatia azimio la Bunge kumuomba Mhe Spika kuwaita mbele ya kamati wakuu wa wilaya na mikoa waliotoa matamshi ya kudharau mamlaka ya Bunge.
Share:

Tuesday 28 March 2017

Polisi Wanaodaiwa Kuiba Mafuta Ya Ndege Wafikishwa Mahakamani

Askari  wawili wanaotuhumiwa kuiba mafuta ya ndege ya Kampuni ya ATCL, kwa kushirikiana na walinzi, wameondolewa kazini na kufikishwa mahakamani kwa tuhuma za uhujumu uchumi.

Washtakiwa hao na wenzao wawili walipandishwa kizimbani jana katika Mahakama ya Hakimu Mkazi Kisutu na kusomewa mashtaka mbele ya Hakimu Mkazi Mkuu, Victoria Nongwa.

Akisoma mashtaka Wakili wa Serikali Mwandamizi, Nassoro Katuga aliwataja washtakiwa hao kuwa ni Koplo Bahati Msilimini (33), PC Benaus (34), Iddi Nyangasa (42) na fundi wa ndege, Ramadhani Mwishehe (52).

Katuga alidai washtakiwa hao wanakabiliwa na mashtaka  mawili, shtaka la kwanza kula njama na shtaka la pili hujuma dhidi ya Serikali.

Alidai katika shtaka la kwanza washtakiwa wanadaiwa kati ya Machi mosi na Machi 17 mwaka huu maeneo ya Uwanja wa Ndege wa Julius Nyerere walikula njama ya kutenda kosa la uhujumu uchumi.

Katika shtaka la pili washtakiwa wote wanadaiwa kati ya tarehe hizo, wakiwa na nia ya kuhujumu manufaa ya Jamhuri ya Muungano ya Tanzania, bila uhalali walitoboa na kuchota mafuta ya ndege lita 280.6 kutoka kwenye ndege JET A1 ya ATCL yenye namba za usajili 5H\MWF-8Q-300.

Katuga alidai kitendo hicho kilizuia utoaji wa huduma muhimu ya usafiri wa ndege.

Hata hivyo wakili huyo alidai upelelezi haujakamilika na hakuna kibali chochote kutoka kwa Mkurugenzi wa Mashtaka nchini (DPP).

Wakili wa utetezi, Martin Rwehumbiza aliiomba mahakama ikubali kuwapa dhamana wateja wake kwa sababu mashtaka yanayowakabili yanadhamana.

Alidai thamani ya mafuta wanayodaiwa kuchota haizidi Sh milioni 10 hivyo mahakama hiyo ina mamlaka ya kutoa dhamana.

Akijibu hoja hiyo Katuga alipinga washtakiwa hao kupewa dhamana kwa madai kwamba wataingilia upelelezi hivyo aliomba wakae ndani kwa muda.

Akitoa uamuzi Hakimu Nongwa alisema sheria inaruhusu Mahakama ya Kisutu kushughulikia dhamana kwa makosa ambayo thamani yake haizidi Sh milioni 10.

“Sirahisi kujua mafuta yalikuwa na thamani gani sababu hayakuwekwa katika hati ya mashtaka, hakuna hati ya kuzuia dhamana kutoka kwa DPP, wangeona washtakiwa wakiwa nje kwa dhamana wataingilia upelelezi wangeweka hati ya kuzuia dhamana zao.

“Dhamana ni haki ya washtakiwa hakuna zuio lolote, mahakama inaona ni vyema washtakiwa wakapewa dhamana, hawawezi kuingilia upelelezi sababu walishaondolewa kazini,”alisema Hakimu Nongwa.

Washtakiwa wote walipata dhamana na wadhamini walitakiwa kuhakikisha washtakiwa hao wanafika mahakamani kila kesi itapokuwepo. Kesi hiyo iliahirishwa hadi Aprili 27 mwaka huu kwa kutajwa.
Share:

Malawi Yaichokonoa Tena Tanzania Kuhusu Ziwa Nyasa


Rais wa Malawi, Peter Mutharika ameanza tena chokochoko baada ya kutangaza kuwa hakuna nchi ambayo inamiliki kwa pamoja Ziwa Nyasa na kwamba haijafikia makubaliano na nchi yoyote, hivyo ameahidi kulinda umiliki na masilahi yake.

Kauli hiyo ni tofauti na mazungumzo ya Mutharika na Rais John Magufuli yaliyofanyika Januari 30 jijini Addis Ababa, Ethiopia wakati walipokuwa wakihudhuria kikao cha Umoja wa Afrika (AU).

Katika taarifa iliyotolewa na Idara ya Mawasiliano ya Rais baada ya kikao hicho, ilisema marais wote wameridhishwa na jitihada zinazofanywa na jopo la usuluhishi lililoteuliwa na Umoja wa Maendeleo wa Nchi za Kusini mwa Afrika (Sadc).

Jopo hilo linaongozwa na rais wa zamani wa Msumbiji, Joachim Chisano.

Mkuu wa kitengo cha mawasiliano katika wizara ya  Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki Mindi Kasiga amekiri kuiona taarifa hiyo na alisema anayeweza kulizungumzia suala hilo ni Naibu Waziri.

“Tumeiona hiyo taarifa ila jaribu kumtafuta Naibu Waziri maana Waziri atakuwa nje ya nchi. Ninachofahamu baraza la usuluhishi bado linaendelea na vikao vyake. Ukimpata naibu waziri atakuwa na maelezo ya kina.”alisema Mindi.

Lakini, akihudhuria Siku ya Maji Duniani Jumatano iliyopita mjini Mangoshi, Rais Mutharika alisisitiza msimamo wa Malawi kulinda umiliki wa ziwa hilo dhidi ya watu aliowaita wavamizi.

Mutharika alisema Malawi ndiye mmiliki pekee wa Ziwa Malawi, ambalo huku linajulikana kama Ziwa Nyasa, na kuonya kuwa utawala wake hautavumilia watu watakaokuwa na nia ya kuyumbisha taarifa za umiliki.

“Hebu tulilinde ziwa letu. Hili ni ziwa letu na ninaposema ziwa letu namaanisha ziwa lote. Mtu yeyote asifanye kosa la kubadili umiliki ambao umekuwepo kwa miaka 124 iliyopita,” alisema Mutharika akikaririwa na tovuti ya Nyasa Times ya Malawi juzi wakati wa mkutano huo uliofanyika ukumbi wa Kituo cha Mikutano cha Nkopola Lakeshore mjini Mangochi.

“Tunathamini ziwa letu na tutahakikisha tunachukua hatua za kulilinda kwa gharama zozote,” alisema.

Mutharika aliwataka wananchi kupunguza matumizi mabaya ya maji ili yapatikane kwa ajili ya kilimo na viwandani wakati wa msimu wa ukame.

Hivi karibuni, Malawi na Tanzania zimejikuta katika mzozo wa umiliki wa Ziwa Nyasa lililo kusini mwa Tanzania, mzozo ambao umesababisha kuanza kwa mazungumzo ya usuluhishi kumaliza kutokubaliana huko baada ya nchi hizo mbili kushindwa kufikia muafaka. Mzozo wa mpaka kwenye Ziwa Nyasa umekuwepo tangu mwaka 1967.

Lakini, mzozo wa hivi karibuni umeibuka baada ya Malawi kuanza utafiti wa mafuta na gesi kwenye ziwa hilo.

Hata hivyo, Mutharika alisema uchimbaji mafuta utaendelea katika ziwa hilo licha ya wanaharakati wa mazingira kuitaka Malawi iache mpango huo.

“Wale wanaohofia kuhusu mipango yetu ya kutafuta na kuchimba mafuta hawana sababu ya kuhofia. Kama tutaamua kuchimba mafuta katika ziwa, tutahakikisha tunatumia teknolojia safi,” alisema akikaririwa na Nyasa Times.
Share:

Ripoti Yathibitisha Faru John alikufa kwa kukosa matunzo

https://i0.wp.com/millardayo.com/wp-content/uploads/2017/03/faru-John.png?resize=660%2C400
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa amepokea taarifa rasmi ya uchunguzi wa kifo cha Faru John kutoka kwa Mkemia Mkuu wa Serikali, Prof. Samwel Manyele ambaye alikuwa akiongoza tume maalum iliyoundwa na Waziri Mkuu.

Akisoma taarifa hiyo mbele ya Waziri Mkuu, Prof. Manyele amesema tume yake ilifanya uchunguzi wa kifo cha Faru John kwa kupima vinasaba vya sampuli mbalimbali vikiwemo mzoga, fuvu, mifupa, pembe, damu, ngozi na kinyesi kilichokaushwa ambapo ilibainika kuwa vyote ni vya mnyama mmoja, aina ya faru mweusi ambaye ni dume.

Prof. Manyele amesema matokeo hayo yamethibitisha kuwa faru John alikufa katika hifadhi ya Sasakwa Grumeti kwa kukosa matunzo na uangalizi wa karibu.

“Maabara iliyotumika ni ya Chuo Kikuu cha Pretoria, Afrika Kusini chini ya usimamizi wa timu ya wataalamu kutoka Tanzania, wachunguzi wa Serikali, chini ya Ofisi ya Mkemia Mkuu wa Serikali. Sababu za kifo chake zilichangiwa na kukosa matunzo na uangalizi wa karibu, kukosa matibabu alipoumwa, mazoea yanayotokana na kutofuata taratibu zilizowekwa kisheria na mapungufu ya kiuongozu kwa Wizara husika, hifadhi na taasisi zake,” amesema.

Prof. Manyele amesema mapungufu waliyoyabaini kutokana na uchunguzi huo ni kutokuwepo kwa kibali rasmi cha kumhamisha Faru John; kukosekana kwa mkataba wa kupokelewa kwa Faru John hifadhi ya Sasakwa Grumeti na kutofuatiliwa kwa afya na maendeleo ya Faru John baada ya kuhamishwa. 

Mengine ni uchukuaji holela wa sampuli za wanyama pori kwa lengo la utafiti na kuzisafirisha nje ya nchi; migongano ya kimaslahi kati ya watumishi waliolenga kusimamia taratibu na wale wenye kusimamia maslahi binafsi na uwepo wa taasisi nyingi zenye mamlaka sawa juu ya masuala ya uhifadhi wa wanyamapori.

“Pamoja na kwamba mawasiliano yanaonyesha zoezi hilo liliridhiwa na Wizara, hapakuwepo na kibali rasmi kutoka kwa Mkurugenzi wa Wanyamapori cha kuruhusu kumhamisha Faru John kutoka NCAA kwenda Grumeti,” amesema Prof. Manyele katika ripoti yake. 

Kwa upande wake Waziri Mkuu ameishukuru timu ya uchunguzi iliyokuwa chini ya Mkemia Mkuu wa Serikali kwa kazi iliyoifanya ikiwemo kuainisha udhaifu uliokuwemo ndani ya Wizara ya Maliasili na Utalii na taasisi zake.

“Ofisi yangu itaipitia taarifa hii ambayo ni kubwa kiasi na kuifanyia kazi. Matokeo ya kazi hiyo, tutayatoa hivi karibuni ili kuonyesha Serikali imeamua kufanya nini juu ya mapendekezo yaliyotolewa.”

Amemtaka mkurugenzi Msaidizi wa Kitengo cha Kupambana na Ujangili wa Wanyamapori, Bw. Robert Mande, afuatilie mapendekezo yaliyoainishwa na tume hiyo na wayafanyie kazi mapema iwezekanavyo
Share:

Nape Akabidhi Ofisi Kwa Mwakyembe

Aliyekuwa Waziri wa Habari Nape  Nnauye amemkabidhi ramsi ofisi Waziri mpya wa Habari, Dkt Harrison George Mwakyembe.
Share:

Total Pageviews

MC ELLY NGWALA

FOR BOOKING PLEASE CALL Business No: +255 713 404 646 +255 784 297 582 +255 767 404 647 Email: mcellyngwala@yahoo.com

MC ELLY NGWALA KTK POZI

My Blog List

Powered by Blogger.

Blog Archive